Halmashauri ya Mji wa Kasulu mkoani Kigoma imeanza kuchukua hatua dhahiri za kuunda msingi imara wa maendeleo endelevu kupitia mipango ya kifedha inayolenga kuboresha huduma, miradi ya jamii, na maisha ya wananchi. Bajeti ya shilingi bilioni 43 kwa mwaka wa fedha 2026/2027, yenye ongezeko la asilimia 14 ikilinganishwa na mwaka uliopita, ni chachu ya mipango hii, ikionyesha dhamira ya halmashauri kuhakikisha kila shilingi inatumika kwa manufaa halisi ya wananchi.
Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji wa Kasulu, Mheshimiwa Ayubu Ngalaba, amesisitiza umuhimu wa uwajibikaji na uwazi katika utekelezaji wa bajeti, wakati wa kikao cha bajeti kilichofanyika leo katika ukumbi wa halmashauri. Kikao hicho kilihusisha Baraza la Madiwani, viongozi wa taasisi mbalimbali, wanajamii, wataalamu kutoka idara mbali mbali za halmashauri, pamoja na Kamati ya Ulinzi na Usalama; kikilenga kukagua mpango wa bajeti, kutoa maoni na mapendekezo, na kuhakikisha vipaumbele vya maendeleo vimezingatiwa kabla ya kupelekwa hatua nyingine.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri, Mwalimu Vumilia Simbeye, ameeleza kuwa maoni na mapendekezo yote yaliyotolewa na Baraza yamezingatiwa na kuyafanyia kazi kabla ya kupelekwa hatua nyingine. “Tunataka miradi yote iliyopangwa ikamilike kwa wakati, bila kusababisha usumbufu kwa wananchi. Kila shilingi iliyopangwa ina lengo la dhati la kuboresha maisha ya wananchi,” alisema.
Wajumbe wa Baraza wamesisitiza kuwa bajeti hii ni chachu ya maendeleo endelevu ya halmashauri. Wameongeza kuwa utekelezaji wake unapaswa kufanyika kwa uwazi, uadilifu, na kuzingatia thamani ya fedha. Wamesema ni wajibu wa kila mtendaji na kiongozi kuhakikisha rasilimali zilizotengwa zinatumika kikamilifu, na miradi inabakia kuwa na athari chanya kwa wananchi kwa muda mrefu.
Mipango hii ya kifedha inaashiria wazi kuwa Halmashauri ya Mji wa Kasulu inajikita katika kujenga msingi imara wa maendeleo endelevu, ikilenga uwajibikaji, uwazi, na matokeo chanya kwa wananchi wake,.