Wananchi wa Halmashauri ya Mji ya Kasulu wamepokea kwa furaha utekelezaji wa Mradi Mkubwa wa maendeleo chini ya mradi wa TACTIC unaofadhiliwa na Benki ya Dunia, ikiwemo ujenzi wa stendi ya kisasa ya mabasi Murusi, uboreshaji wa Soko Kuu la Kumsenga na ujenzi wa barabara ya kilomita 5.7 inayounganisha kata za Murusi na Murubona.
Katika kikao cha wadau kilichofanyika leo na kuhudhuriwa na viongozi wa serikali, wataalam kutoka Halmashauri ya Mji Kasulu, wajasiriamali wadogo wa stendi ya sasa ya Murusi, pamoja na uongozi wa stendi. Washiriki walipata nafasi ya kuchangia maoni kuhusu jinsi wanavyotamani stendi mpya iwe – wakieleza mahitaji muhimu kama vile huduma za vyoo vya kisasa, maegesho ya kisasa, mabanda ya biashara, usalama, taa za barabarani, na huduma za kifedha.
Katika kata ya Kumsenga, kikao sawa kilifanyika kwa ajili ya maandalizi ya uboreshaji mkubwa wa soko la eneo hilo, hatua inayotarajiwa kuinua biashara na kipato cha wananchi wa maeneo husika.
Kwa upande mwingine TACTIC pia itajenga barabara mpya ya kuunganisha eneo la Makaburini – Hwaz Secondary – Kibondo road kupitia Ngondano, yenye urefu wa kilomita 5.7, jambo litakalosaidia kupunguza gharama za usafiri na kukuza shughuli za kiuchumi.
Diwani wa Kata ya Murusi, Mheshimiwa Phanuel Eliabi Kisabo, alielezea matumaini makubwa ya wananchi kuhusu mradi huu. Alisema:
“Mradi huu ni kama tumaini jipya kwa wananchi wa Murusi. Tunamshukuru Rais Samia kwa kusikiliza kilio cha wananchi wa chini. Tunatamani utekelezaji uanze haraka ili wajasiriamali wetu wapate mazingira bora ya kufanyia kazi na kuendesha familia zao.”
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Kasulu naye alitoa shukrani kwa Serikali ya Awamu ya Sita kwa kuendelea kuleta miradi ya maendeleo yenye manufaa kwa wananchi. Aliongeza:
“Tunawashukuru pia wananchi kwa ushiriki wao wa hali ya juu katika vikao hivi. Ushirikishwaji huu ni msingi wa mafanikio ya miradi ya aina hii. Hivyo, tunawahimiza waendelee kushiriki katika hatua zote zinazofuata.”
Kwa upande wa timu ya washauri wa mradi, Sweetheart Mlowe, kiongozi wa timu kutoka kampuni ya Interconvert inayosimamia usanifu wa miundombinu, alitoa shukrani zake kwa ushirikiano mkubwa walioupata kutoka kwa viongozi na wananchi. Alisema:
“Leo tumekuja kupokea maoni kutoka kwa wanufaika wa miradi. Ushirikiano tulioupata ni wa kupongezwa, na tumevutiwa sana na jinsi wananchi walivyochangia kwa uwazi na kujali maendeleo ya eneo lao. Tunawaomba viongozi waendelee kushirikiana nasi katika hatua zinazofuata, kwani baada ya hapa tutayapitia maoni haya kwa kina na baadaye tutarudi tena kwa wananchi kuonyesha kile tunachokusudia kukitekeleza.”
Kazi na Utu, Tunasonga Mbele.