Leo, Halmashauri ya Mji Kasulu imeendesha mafunzo ya Mfumo wa MUKI kwa waajiriwa wapya kutoka kada mbalimbali. Mafunzo haya yalifanyika katika ukumbi mkubwa wa Halmashauri na yaliwezeshwa na Maafisa TEHAMA pamoja na Maafisa Utumishi.
Akifungua mafunzo hayo, Mkuu wa Idara ya Utumishi, Bw. Nyemo John Mbogoni, aliwasisitiza waajiriwa wapya kuhakikisha wanaelewa vizuri mfumo wa MUKI, akieleza kuwa mafunzo haya ni muhimu sana kwao kama waajiriwa wapya. Alisisitiza umuhimu wa kuendana na teknolojia ya kisasa, kwani shughuli nyingi za kiutumishi sasa zinafanyika kwa njia ya kidigitali kupitia mifumo mbalimbali.
Kwa upande wake, mwezeshaji wa mafunzo, Ndg. Charles Joseph Nyanyembe, alieleza kuwa mafunzo haya yamelenga kuwajengea uwezo watumishi wapya ili wanapoanza kazi waweze kuelewa kanuni na miongozo ya serikali.
Washiriki wa mafunzo walitoa shukrani kwa uongozi wa Halmashauri kwa kuwapatia mafunzo haya. Amiri Dhafa Hatibu, mwajiriwa mpya katika kada ya Elimu, alisema, “Tulivyokuja si kama tulivyoondoka,” akimaanisha kuwa mafunzo hayo yamewapa uelewa mkubwa. Leonatha Ndimbo, mwajiriwa mpya katika kada ya Ufarmasia, alieleza kuwa kutokana na mabadiliko makubwa ya kiteknolojia, mafunzo haya yamewasaidia kuelewa na kuendana na teknolojia hiyo.
Kwa taarifa zaidi kuhusu shughuli za Halmashauri ya Mji Kasulu, unaweza kutembelea tovuti yao rasmi: kasulutc.go.tz.